Faida za kuwa na Blogu kwa watu binafsi


Blogu siyo kitu kigeni masikioni mwa watumia mtandao, wengi wetu hutembelea blogu kila siku kupata habari, burudani n.k. Blogu sasa zimeanza kuwapatia kipato wanaoendesha blogu zao kwa ufanisi mfano Issa Michuzi.  Kwenye makala hii nitaongelea kuhusu Blogu, sababu zinazofanya watu binafsi kuanzisha blogu, faida zake na nini cha kufanya kuweza kuanzisha na kunufaika na blogu.

Blogu ni nini?
Blogu ni aina ya tovuti ambayo makala zake hupangwa katika mpangilio unaoanza na makala mpya juu ya ukurasa mkuu (home page) na makala za zamani zikielekea chini. Tofauti kati ya blogu na tovuti za aina nyingine mfano tovuti ya gazeti la mwananchi (tovuti tuli “static”) au jamii forum (tovuti jukwaa “forum”) ni hizi zifuatazo.

  1. Maudhui ya blogu (makala, picha, video n.k.)hupangwa kwa kuanza na maudhui mapya yakiwa juu ya ukurasa mkuu halafu maudhui ya zamani yakielekea chini.
  2. Maudhui ya blogu huongezwa mara kwa mara
  3. Wanaotembelea blogu wanaweza kuacha maoni yao kuhusu maudhui au blogu kwa ujumla.
Zipo tofauti nyingine lakini hizi zilizo ainishwa hapo juu kwa pamoja ndiyo zina tofautisha blogu na tovuti nyingine.

Kwa nini watu wanaanzisha blogu?
Watu huanzisha blogu kwa sababu mbali mbali ila kuna sababu ambazo husukuma watu wengi kuanzisha blogu zao binafsi.

Kufundisha; Watu wengi wenye utaalamu au ujuzi na jambo fulani huanzisha blogu kwa ajili ya kufundisha. Mfano mtu anayefanya kazi kwenye duka la kuuzia simu anaweza kuanzisha blogu ya kusaidia watu kutambu simu feki au simu zitakazo kidhi mahitaji au utunzaji bora wa simu yako n.k.
Kusaidia; Kuna watu wanaoanzisha blogu kwa ajili ya kusaidia watu. Mfano daktari anaweza kuanzisha blogu ya kusaidia watu na matatizo yao ya kiafya.

Kipato; Pia wapo watu ambao huanzisha blogu kama njia ya kujipatia kipato. Hapa kuna kuwa na tofauti kati ya blogu moja na nyingine, wapo wanaouza bidhaa kupitia blogu zao, wapo wanaouza ujuzi wao n.k
Hizi ni baadhi ya sababu kubwa zinazo pelekea watu binafsi kuanzisha blogu lakini siyo sababu pekee.

Faida za kuwa na blogu
Faida za kuwa na blogu ni nyingi kwa wale ambao wana tafuta njia mbadala ya kufikisha ujembe wao kwa haraka, urahisi na unafuu. Baadhi ya faidi kubwa za kuwa na blogu ni;

Blogu ni rahisi kuanzisha na kusimamia; Kuanzisha blogu ni rahisi sana na inachukua chini ya dakika 5 kuanzisha blogu yako bila gharama yeyote zaidi ya kuwa na mtandao. Vile vile kuendesha na kusimamia blogu yako ni rahisi kwani unaweza kuweka makala zako mtandaoni kwa kutumia simu, barua pepe n.k.

Ni rafiki wa search engine; Zaidi ya nusu ya watu wote wanaotumia mtandao duniani hutumia search engines kutafuta makala mtandaoni. Ukiweza kutumia blogu yako vizuri unaweza kufaidika na utitiri wa watu wanaotumia search engines. Blogu tofauti na tovuti zingine inauwezo mkubwa wa kufaidika na search engine ambayo itakuletea wageni wengi ukiitumia vizuri.

Blogu huvuta wageni wengi; Uwezo mkubwa wa kutumia search engines, uhamasishaji wa ushiriki kwa kutoa maoni unasaidia blogu kuvutia watu wengi kuliko tovuti nyingine. Ukiweza kuweka makala zenye mvuti, zenye kuhabarisha, kuelimisha, kuburudisha n.k. hutakosa wageni kwenye Blogu yako mfano Blogu ya Issa Michuzi, ni maarufu si kwa sababu ya Michuzi bali ni kwa sababu ya maudhui yake.

Blogu itakupatia kipato; Ukiweza kuwa na maudhui yenye mzuti, ukatumia search
engine vizuri utapata wageni wengi kwenye blogu yako. Ukiwa na watu wengi wanaotembelea blogu yako, watu, makampuni nakadhalika watataka kuwafikia wageni wanaotembelea blogu yako. Njia ya kuwafikia ni matangazo ambayo itabidi wakulipe hivyo kukuingia kipato.  

Blogu inaweza kukupatia ajira; Kwa wale ambao hawana ajira na wanaujuzi fulani au wamesomea kitu Fulani, blogu inaweza kuwa njia ya kukupatia ajira. Mfano umesomea ubunifu wa majengo na huna ajira unaweza kuanzisha blogu ambayo inatoa ushauri kuhusu namna bora ya ujenzi bure. Na kama maudhui ya blogu yako yatasaidia watu kujenga nyumba bora, kuokoa fedha n.k. (i) Utapata watu wengi watakaotembelea blogu yako kwa ajili ya kupata ushauri (makampuni ya bidhaa za ujenzi yatataka kufikia wageni wa blogu yako kupitia matangazo). (ii) Ushauri wako unakuwa ni sehemu ya C.V. yako hivyo kuongeza uwezekano wa kupata ajira.   

Sehemu ya kuanzia
Kabla hujaanzisha blogu yako hakikisha unajibu maswali matatu muhimu, (1) Je unaielewa vizuri mada utakayozungumzia kwenye blogu yako? e.g. Soka, siasa, mitindo n.k. (2) Unaipenda mada ya blogu yako kiasi cha kuweza kuifanya bila malipo? (3) Je unauvumilivu utakaouhitaji kufikisha blogu yako mahali ambapo unataka? Ukiweza kujibu maswali haya matatu kwa ufasaha basi uwezekano wa kuwa na blogu yenye mafanikio unaongezeka maradufu.

Unapoanzisha blogu yako kuna mambo muhimu ya kuzingatia (haya ni baadhi tu) (a) Lazima maudhui yako yawe na mvuto (b) Uwekaji wa makala kwenye blogu yako lazima uwe unatabirika (mfano utaweka makala mara moja kwa siku, wiki n.k.) (c) Lazima usambaze makala za blogu yako kwenye mitandao ya jamii, blogu marafiki, mtandaoni (hapa ni muhimu kutumia njia yeyote ya kihalali) (d) Lazima uwe mdadisi wa mbinu mbali mbali za kukuza blogu yako (Ukituumia Google utapata makala nyingi zitakazo weza kusaidia katika hili).

Kuanzisha blogu yako leo bure nenda kwenye jukwaa la Blogger, hakikisha una akaunti ya barua pepe ya Gmail. Kama huna nenda Gmail ujisajili bure, halafu tumia akaunti yako ya Gmail kusajili Blogu yako. Fuata maelekezo ya kuanzisha blogu na ndani ya dakika 5 utakuwa na blogu yako tayari kuanza kuweka makala zako mtandaoni.

Vile vile unaweza kututembelea kwa kuingia hapa kuona huduma ambazo tunaweza kukupa kusaidia blogu yako ifanikiwe.